1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUrusi

Urusi yadai kukamata vijiji sita mashariki mwa Ukraine

Tatu Karema
11 Mei 2024

Urusi imesema leo kuwa imeviteka vijiji sita mashariki mwa Ukraine wakati wa mashambulizi ya kushtukiza yaliyosababisha kuhama kwa watu wengi.

https://p.dw.com/p/4fkAP
Mapambano katika vita vya Ukraine
Mapambano katika vita vya Ukraine. Picha: ANATOLII STEPANOV/AFP

Hayo yanajiri wakati Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky akitoa wito wa haraka wa msaada wa kijeshi.

Wizara ya ulinzi ya Urusi imesema wanajeshi wake "wamekomboa" vijiji vitano vya  Borysivka, Ogirtseve, Pletenivka, Pylna na Strilecha katika mkoa wa Kharkiv nchini Ukraine unaopakana na nchi hiyo .

Wizara hiyo imeendelea kusema kuwa kijiji cha Keramik katika mkoa wa Donetsk, sasa pia kiko chini ya udhibiti wa Urusi.

Maafisa wa Ukraine wamesema kuwa vikosi vya nchi hiyo vimetoa upinzani mkali lakini mapigano ni makali katika eneo hilo la Kharkiv.

Hata hivyo kupitia ujumbe kwenye mitandao ya kijamii, gavana wa jimbo la Kharkiv Oleg Synegubov amesisitiza kuwa hakuna kitisho cha mashambulizi ya ardhini mjini humo.